“Yehova mwenyewe asipoijenga nyumba, ni bure kwamba wajenzi wake wameifanyia kazi ngumu.”—ZAB. 127:1a.
1-3. Wenzi wa ndoa wanakabili changamoto gani? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)
MUME
ambaye amekuwa na ndoa yenye furaha kwa miaka 38 anasema hivi:
“Mkijitahidi kabisa kwa unyoofu na kuonyesha kwamba mnataka ndoa yenu
ifanikiwe, Yehova atawabariki.” Naam, waume na wake wanaweza kuwa na
ndoa yenye furaha na pia kutegemezana nyakati za taabu.—Met. 18:22.
2 Hata hivyo, ni kawaida kwa wenzi wa ndoa kupata “dhiki katika mwili wao.” (1 Kor. 7:28)
Kwa nini? Kwa sababu, kushughulika na matatizo ya maisha kunaweza
kusababisha mkazo katika ndoa. Kwa kuwa mume na mke si wakamilifu
nyakati nyingine wanaumizana hisia, wanakosana, au kutoelewana, na hali
hizo zinaweza kusababisha matatizo hata katika ndoa ambazo ni bora. (Yak. 3:2, 5, 8)
Wenzi wengi wa ndoa wana shughuli nyingi sana za kazi huku wakitunza
watoto wao. Mkazo na uchovu hufanya iwe vigumu kwa wenzi fulani wa ndoa
kupata wakati wanaohitaji ili kuimarisha ndoa yao. Matatizo ya kifedha,
matatizo ya kiafya, au magumu mengine huenda yakadhoofisha upendo na
heshima kati yao. Isitoshe, msingi wa ndoa iliyoonekana kuwa imara
unaweza kudhoofishwa na “matendo ya mwili,” kama vile uasherati, mwenendo mpotovu, uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, na magomvi.—Gal. 5:19-21.
3 Hali ni mbaya zaidi kwa sababu katika “siku za mwisho” watu ni wachoyo na hawamwogopi Mungu, mambo ambayo ni sumu katika ndoa. (2 Tim. 3:1-4)
Isitoshe, adui mwenye hila ameazimia kuishambulia ndoa. Mtume Petro
anatuonya hivi: “Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba
anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.”—1 Pet. 5:8; Ufu. 12:12.
4. Wenzi wa ndoa wanawezaje kujenga ndoa imara na yenye furaha?
4 Mume
fulani nchini Japani anakiri hivi: “Nilikuwa na mkazo mkubwa kwa sababu
ya matatizo ya kifedha. Na mke wangu alipata pia mkazo mkubwa kwa
sababu hatukuwa na mawasiliano mazuri. Pia, hivi karibuni alipata
matatizo makubwa ya kiafya. Nyakati nyingine, tuligombana kwa sababu ya
mkazo huo.” Kuna matatizo ambayo hayaepukiki katika ndoa, lakini
yanaweza kutatuliwa. Kwa msaada wa Yehova, wenzi wa ndoa wanaweza kuwa
na ndoa imara na yenye furaha. (Soma Zaburi 127:1.) Acheni
tuzungumzie mambo matano ambayo ni kama mawe ya kiroho yanayojenga ndoa
imara na inayodumu. Kisha tutachunguza jinsi mambo hayo yanavyoweza
kuunganishwa kwa upendo.
MWEKENI YEHOVA KATIKA NDOA YENU
5, 6. Waume na wake wanaweza kufanya nini ili Yehova awe katika ndoa yao?
5 Msingi wa kujenga ndoa salama ni ushikamanifu na ujitiisho kwa Mwanzilishi wa ndoa. (Soma Mhubiri 4:12.) Waume
na wake wanaweza kumweka Yehova katika ndoa yao kwa kufuata mwongozo
wake wenye upendo. Biblia inasema hivi kuhusu watu wa kale wa Mungu:
“Masikio yako yatasikia neno nyuma yako likisema: ‘Hii ndiyo njia.
Tembeeni ndani yake,’ iwe mtakwenda upande wa kuume au iwe mtakwenda
upande wa kushoto.” (Isa. 30:20, 21) Leo, wenzi wa ndoa wanaweza ‘kusikia’ neno la Yehova kwa kusoma Neno la Mungu pamoja. (Zab. 1:1-3)
Wanaweza kuimarisha zaidi ndoa yao kupitia programu ya Ibada ya Familia
inayofurahisha na kuburudisha kiroho. Pia, kusali pamoja kila siku ni
muhimu sana katika kujenga ndoa inayoweza kustahimili mashambulizi ya
ulimwengu wa Shetani.
Wenzi
wa ndoa wanapofanya mambo ya kiroho pamoja, wanakuwa na uhusiano wa
karibu na wenye furaha pamoja na Mungu na kati yao (Tazama fungu la 5,
6)
6 Gerhard
anayeishi Ujerumani anasema hivi: “Wakati wowote shangwe yetu
inapoathiriwa na matatizo au kutoelewana, ushauri wa Neno la Mungu
umetusaidia kusitawisha subira na kusameheana. Hizo ni sifa muhimu sana
katika ndoa yenye mafanikio.” Wenzi wa ndoa wanapojitahidi kumweka Mungu
katika ndoa yao kwa kushiriki utendaji wa kiroho pamoja, wanakuwa na
uhusiano wa karibu na wenye furaha pamoja na Mungu na kati yao.
WAUME—TUMIENI UKICHWA KWA UPENDO
7. Waume wanapaswa kutumiaje ukichwa wao?
7 Jinsi
mume anavyotumia ukichwa wake kunaweza kumsaidia sana kujenga ndoa
imara na yenye furaha. Biblia inasema hivi: “Kichwa cha kila mwanamume
ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” (1 Kor. 11:3)
Muktadha wa maneno hayo unawaonyesha waume jinsi wanavyopaswa kutumia
ukichwa wao—kama Kristo anavyotumia mamlaka yake juu ya mwanamume. Yesu
hakuwa kamwe mtawala wa mabavu au mkali, sikuzote alikuwa mwenye upendo, fadhili, usawaziko, tabia-pole, na mnyenyekevu moyoni.—Mt. 11:28-30.
8. Mume anaweza kufanya nini ili aheshimiwe na kupendwa na mke wake?
8 Waume
Wakristo hawahitaji kudai tena na tena wake zao wawaheshimu. Badala
yake, ‘wanaendelea kukaa nao vivyo hivyo kulingana na ujuzi,’ yaani,
kuwafikiria na kuwaelewa. ‘Wanawapa heshima kama chombo dhaifu zaidi,
yaani, mwanamke.’ (1 Pet. 3:7) Waume huonyesha hadharani na faraghani kwa maneno ya heshima na matendo ya fadhili kwamba wake zao ni wenye thamani kwao. (Met. 31:28) Mume anayetumia ukichwa wake kwa njia hiyo ya upendo ataheshimiwa na kupendwa na mke wake, na Mungu atabariki ndoa yao.
WAKE—JITIISHENI KWA UNYENYEKEVU
9. Mke anawezaje kujitiisha kwa unyenyekevu?
9 Upendo usio wa kichoyo na unaotegemea kanuni kumwelekea Yehova hutusaidia sote kujinyenyekeza chini ya mkono wake wenye nguvu. (1 Pet. 5:6)
Njia moja muhimu ambayo mke mwenye ujitiisho anaonyesha kwamba
anaheshimu mamlaka ya Yehova ni kwa kushirikiana na kumuunga mkono mume
wake. Biblia inasema hivi: “Enyi wake, jitiisheni kwa waume zenu, kwa
kuwa inafaa katika Bwana.” (Kol. 3:18)
Kihalisi, mke hatafurahia maamuzi yote ya mume wake. Hata hivyo, ikiwa
maamuzi ya mume hayakiuki sheria za Mungu, basi mke mnyenyekevu yuko
tayari kumuunga mkono.—1 Pet. 3:1.
10. Kwa nini ni muhimu kwa wake kujinyenyekeza kwa upendo?
10 Mke ana jukumu la heshima akiwa ‘mwenzi’ wa mume wake. (Mal. 2:14)
Anatoa maoni muhimu kuhusu maamuzi ya familia. Anafanya hivyo kwa
kueleza kwa heshima mawazo na hisia zake lakini kwa unyenyekevu. Mume
mwenye hekima atasikiliza kwa makini maoni ya mke wake. (Met. 31:10-31) Mke anapojitiisha kwa upendo familia inakuwa na shangwe, amani, na umoja, na waume na wake wanaridhika kwa sababu wanajua kwamba wanampendeza Mungu.—Efe. 5:22.
ENDELEENI KUSAMEHEANA KWA HIARI
11. Kwa nini ni muhimu kusameheana?
11 Msamaha
ni kati ya mambo muhimu sana yanayojenga ndoa yenye kudumu. Ndoa
huimarika wakati waume na wake ‘wanapoendelea kuvumiliana na kusameheana
kwa hiari.’ (Kol. 3:13)
Kinyume chake, ndoa hudhoofika wakati wenzi wa ndoa wanapoendelea
kukumbuka makosa ya zamani na kuyatumia kila mara kushambuliana. Kama
vile nyufa zinavyoweza kudhoofisha jengo, ndivyo manung’uniko na
kinyongo kinavyoweza kusitawi moyoni mwetu na kufanya iwe vigumu zaidi
kusamehe. Lakini ndoa huimarika zaidi wakati mume na mke
wanaposameheana, kama Yehova anavyowasamehe.—Mika 7:18, 19.
12. Upendo hufunika “dhambi nyingi” jinsi gani?
12 Upendo wa kweli “hauweki hesabu ya ubaya.” Nao “hufunika dhambi nyingi.” (1 Kor. 13:4, 5; soma 1 Petro 4:8.) Yaani,
tukiwa na upendo hatutaweka mpaka wa idadi ya makosa tunayoweza
kusamehe. Mtume Petro alipouliza ni mara ngapi alipaswa kusamehe, Yesu
alimjibu hivi: “Mpaka mara 77.” (Mt. 18:21, 22) Yesu alikuwa akionyesha kwamba Mkristo anapaswa kuwasamehe wengine bila kikomo.—Met. 10:12. *
13. Tunawezaje kushinda mwelekeo wa kutosamehe?
13 Annette
anasema hivi: “Ikiwa wenzi wa ndoa hawataki kusameheana, kinyongo na
kutoaminiana husitawi na mambo hayo ni sumu katika ndoa. Kusameheana
huimarisha ndoa yenu na kuwasaidia kukaribiana zaidi.” Ili kuepuka
mwelekeo wa kutosamehe, jitahidi kuwa na mtazamo wa kushukuru na
kuthamini. Uwe na zoea la kumpongeza mwenzi wako kutoka moyoni. (Kol. 3:15) Mkifanya hivyo, mtakuwa na umoja, mtapata amani ya akili na baraka ambazo Mungu huwapa wale wanaosamehe.—Rom. 14:19.
TUMIENI ILE KANUNI BORA
14, 15. Ile Kanuni Bora ni nini, na kuitumia kunaimarishaje ndoa?
14 Bila
shaka, unapenda kutendewa kwa heshima na staha. Unathamini watu
wanapotilia maanani maoni na hisia zako. Lakini je, umewahi kumsikia mtu
akisema, “Dawa ya moto ni moto”? Ingawa nyakati nyingine itikio hilo
linaeleweka, Biblia inatuambia hivi: “Usiseme: ‘Nitamtendea kama vile tu alivyonitendea.’” (Met. 24:29)
Kwa kweli, Yesu alipendekeza njia nzuri zaidi ya kushughulikia hali
ngumu. Kanuni hiyo ya mwenendo huitwa mara nyingi ile Kanuni Bora.
Inasema hivi: “Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni
wao vivyo hivyo.” (Luka 6:31) Yesu alimaanisha kwamba tunapaswa kuwatendea watu jinsi ambavyo tungependa kutendewa
na kutolipa ubaya kwa ubaya. Inamaanisha kwamba ikiwa tunataka ndoa
yetu iwe na sifa fulani tunahitaji kusitawisha sifa hiyo.
15 Watu
waliofunga ndoa huimarisha uhusiano wao wanapojali hisia za mwenzi wao.
Mume mmoja nchini Afrika Kusini anasema hivi: “Tumejitahidi kutenda
kulingana na ile Kanuni Bora. Ni kweli
kwamba nyakati nyingine tunakasirika, lakini tumejitahidi kutendeana
jinsi ambavyo tungependa kutendewa—kwa heshima na staha.”
16. Mume au mke hapaswi kumfanyia nini mwenzi wake?
16 Usitangaze
udhaifu wa mwenzi wako wa ndoa au kusema-sema kuhusu kasoro zake, hata
kwa njia ya mzaha. Kumbuka kwamba ndoa si shindano la kujua ni nani
mwenye nguvu zaidi, au ni nani anayeweza kupaaza sauti ya juu zaidi, au
ni nani anayeweza kusema maneno yenye kuumiza zaidi. Ni kweli kwamba
sote tuna kasoro, na nyakati nyingine tunawakasirisha wengine. Lakini
hakuna sababu yoyote kwa mume au mke kutumia dhihaka, maneno ya dharau,
au matusi, kupambana au kupigana na mwenzi wake.—Soma Methali 17:27; 31:26.
17. Waume wanawezaje kuishi kulingana na ile Kanuni Bora?
17 Hata
ingawa katika tamaduni fulani wanaume wanaowakandamiza au kuwapiga wake
zao huonwa kuwa mashujaa, Biblia inasema hivi: “Asiye mwepesi wa hasira
ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu, naye anayezuia roho yake ni bora kuliko mtu anayeteka jiji.” (Met. 16:32)
Ili kumwiga Yesu Kristo, yule mwanamume mkuu zaidi aliyewahi kuishi
duniani, mtu anahitaji kuwa na nguvu nyingi za kimaadili na kuzuia roho
yake. Mwanamume anayemuumiza kwa maneno au kimwili mke wake si shujaa
hata kidogo, na atapoteza uhusiano wake na Yehova. Mtunga-zaburi Daudi,
aliyekuwa mwanamume mwenye nguvu na jasiri, alisema hivi: “Fadhaikeni,
lakini msitende dhambi. Semeni moyoni mwenu, kitandani mwenu, na
kunyamaza.”—Zab. 4:4.
“JIVIKENI UPENDO”
18. Kwa nini ni muhimu kuendelea kusitawisha sifa ya upendo?
18 Soma 1 Wakorintho 13:4-7. Upendo
ni sifa muhimu zaidi katika ndoa. “Jivikeni upendo mwororo wenye
huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Lakini,
zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo
kikamilifu cha muungano.” (Kol. 3:12, 14)
Upendo wa kujidhabihu kama wa Kristo ni kama saruji inayounganisha mawe
ya mfano yanayojenga ndoa imara. Upendo huo hufanya ndoa isivunjike
hata mwenzi wa ndoa akiwa na kasoro zenye kuudhi, matatizo makubwa ya
kiafya, matatizo ya kifedha yanayosababisha mkazo, na matatizo na wakwe.
19, 20. (a) Wenzi wa ndoa wanawezaje kufanikiwa kujenga ndoa imara na yenye furaha? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?
19 Kwa
kweli, ili ndoa ifanikiwe, waume na wake wanahitaji kujitoa kwa upendo,
kuwa washikamanifu, na kujitahidi kabisa. Badala ya kukimbia ndoa
matatizo yanapotokea, wenzi wa ndoa wanapaswa kuazimia kuboresha
uhusiano wao badala ya kuvumiliana tu. Wenzi Wakristo wanaompenda Yehova
na kupendana wanachochewa na upendo wao kwa Mungu na kati yao kutatua
matatizo yao, kwa kuwa “upendo haushindwi kamwe.”—1 Kor. 13:8; Mt. 19:5, 6; Ebr. 13:4.
20 Ni vigumu sana kujenga ndoa imara na yenye furaha katika ‘nyakati ngumu’ tunamoishi. (2 Tim. 3:1)
Lakini inawezekana kwa msaada wa Yehova. Hata hivyo, wenzi wa ndoa
wanapaswa pia kupambana na maadili mapotovu yaliyoenea katika ulimwengu
huu. Makala inayofuata itazungumzia mambo ambayo waume na wake wanaweza
kufanya ili kuimarisha ndoa yao kiroho.